Wednesday, October 26, 2011

JAHAZI MORDEN TAARAB INAKULETEA USIKU WA BABA NA MWANA.

 MFALME MZEE YUSSUF AKIWA NA ISHA MASHAUZI
 ISHA MASHAUZI 'DUME LA SIMBA' AKIWA KATIKA POZI
HAPA NI MZEE YUSSUF.

WAKALI WA MUZIKI WA TAARAB NCHINI, JAHAZI MORDEN WANAKULETA ONYESHO MAALUMU LITAKALOFANYIKA JUMAPILI HII KATIKA UKUMBI TRAVETINE MAGOMENI.

ONYESHO HILO LILILOPEWA JINA LA USIKU WA BABA NA MWANA LITAWAKUTANISHA ISHA MASHAUZI NA MZEE YUSSUF AMBAO WATALISHAMBULIA JUKWAA SIKU HIYO.

WAIMBAJI HAO MAHIRI KATIKA TASNIA YA TAARAB WAMEAHIDI KUTOA BURUDANI YA NGUVU SIKU HIYO NA WAMEWAOMBA WAPENZI NA MASHABIKI KUJITOKEZA KWA WINGI SIKU HIYO.

Monday, February 28, 2011

MAKATIBU WAKUU WA WIZARA HAOOO

Rais Jakaya Kikwete amefanya uteuzi wa Makatibu Wakuu watano wapya na kuwahamisha wengine wanne kutoka wizara moja kwenda nyingine.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana  na Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo, uteuzi na uhamisho huo unaanza mara moja.

Taarifa hiyo imeeleza kwamba mabadiliko hayo yametokana na muundo mpya wa Serikali ambako Wizara ya Miundombinu imegawanywa katika wizara mbili, na baadhi ya Makatibu Wakuu kustaafu kazi kwa mujibu wa sheria.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Rais Kikwete amemteua  Fanuel E. Mbonde kuwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Ikulu. Kabla ya uteuzi Mbonde alikuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu.

Wengine walioteuliwa ni Hussein  Kattanga - Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa; John M. Haule - Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Herbert Mrango - Wizara ya Ujenzi na  Eric K. Shitindi - Wizara ya Kazi na Ajira.

Kabla ya uteuzi wake  Kattanga alikuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto. Haule alikuwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha,  Mrango alikuwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi , Shittindi alikuwa Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma.

Kwa upande wa waliobadilishwa vituo vyao, Rais Kikwete amemhamisha  Sazi  Salula kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kwenda Ofisi ya Makamu wa Rais, Maimuna  Tarishi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kwenda Wizara ya Maliasili na Utalii.

Pia  Injinia Omar  Chambo anahamia Wizara ya Uchukuzi akitokea Wizara ya zamani ya Miundombinu na Kijakazi  Mtengwa -anakuwa Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto.

Taarifa ilieleza kwamba  kuwa Dk. Ladislaus  Komba, aliyekuwa Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii anapangiwa kazi maalum katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.

Aidha,  Rais Kikwete amemhamishia  Elizabeth  Nyambibo Wizara ya Fedha na Uchumi ambako anachukua nafasi ya Naibu Katibu Mkuu iliyoachwa wazi na  Haule. Kabla ya uhamisho  Nyambibo alikuwa Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo  Makatibu Wakuu wanatarajia kuapishwa  leo saa tatu  Machi
00000


Sunday, February 20, 2011

WATANZANIA TUACHANE NA FIKRA ZA KUAJIRIWA, TUWAZE KUJIAJIRI

NA EPSON LUHWAGO
WAHITIMU wa kada mbalimbali nchini, wametakiwa kuondokana na dhana ya kuajiriwa pindi wanapomaliza masomo yao na badala yake wafikirie kujiajiri.
Rai hiyo ilitolewa jana na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi nchini (TPSF), Godfrey Simbeye, wakati wa mahafali ya pili ya kidato cha sita katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Ghomme, iliyoko Ununio nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam.
Simbeye alisema Watanzania wengi wanapomaliza masomo yao, hufikiria kuajiriwa, jambo ambalo linasababisha miongoni mwao kukosa ajira kwa vile nafasi za kazi ni chache.
“Watanzania wanafikiria kujiajiri baada ya kustaafu, sasa tujitahidi kubadilisha mawazo haya ili twende na wakati wa sasa,” alisema.
Alisema Watanzania waanze kubadilika na kufikiria kujiajiri badala ya kuajiriwa kwa sababu hivi sasa fursa ziko nyingi zinazotoa mwanya wa kujitegemea.
Naye Mkurugenzi wa Shule, Dk. Emmanuel Malangalila, alisema licha ya kuwa na muda mfupi tangu kuanzishwa, shule hiyo imekuwa na mafanikio makubwa kitaaluma.
Alisema katika matokeo ya kidato cha sita mwaka jana, wanafunzi wanne waliohitimu walifaulu na kuchaguliwa kujiunga na vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu.
Kwa upande wa kidato cha nne mwaka jana, Dk. Malangalila alisema wanafunzi wote 20 waliofanya mtihani walifaulu na wanatarajiwa kujchaguliwa kuingia kudato cha tano.
Katika mahafali hayo, jumla ya wanafunzi 12 walihitimu kidato cha sita na Mkurugenzi huyo alisema kutokana na rekodi za kitaaluma, ana matumaini kuwa wote watafaulu na kuendelea na masomo ya elimu ya juu

GEORGE MLAWA ACHARUKA

NA EPSON LUHWAGO
KATIBU wa zamani wa Bunge, George Mlawa, ameshauri serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa elimu, kufanya uchunguzi wa kina kuhusu wanafunzi wengi kufeli mtihani wa kidato cha nne.
Akizungumza wakati wa mahafali ya kidato cha sita katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Ghomme, Dar es Salaam, juzi, Mlawa alisema serikali inatakiwa kuchukua hatua madhubuti kwa sababu matokeo hayo kwa mwaka jana, hayana ishara nzuri.
“Kama zaidi ya asilimia 88 ya wanafunzi wamepata daraja la nne na sofuri, hapo yapo matatizo makubwa na si suala la kunyamazia au kutoa majibu rahisi hata kidogo,” alisema.
Kwa mtazamo wake, alisema tatizo linalofanya wanafunzi wengi kufeli ni kushindwa kumudu Kiingereza ambayo ni lugha ya kufundishia kuanzia kidato cha kwanza hadi cha sita.
Alisema wanafunzi wengi wanaoingia kidato cha kwanza wanaanza kujifunza masomo kwa Kiingereza katika hatua hiyo, jambo ambalo anafikiri inakuwa vigumu kuimudu.
Kutokana na hali hiyo, alisema wanafunzi wanakuwa hawako tayari kukabiliana na masomo hivyo ni vyema serikali na wadau wakakaa na kujadili kama kuna uwezekano wa kuamua kufundisha masomo yote kwa Kiswahili kasoro somo la Kiingereza.
“Ukienda China, Russia na Ujerumani wanafunzi wanalazimishwa kutumia lugha za mataifa hayo. Kwa nini nasi tusitumie Kiswahili kama wenzetu? Hiyo ni changamoto kwangu kwa serikali na wadau wa elimu,” alisema.
Hata hivyo, alisema kwa shule za mchepuo wa Kiingereza zinaweza kuamua kutumia lugha hiyo kwa kuwa zimeshawajenga wanafunzi wao na wengi wanaijua vyema.
Mbali na lugha, Mlawa alisema tatizo lingine ni Baraza la Taifa la Mitihani (NECTA) kuwataka wanafunzi wanaorudia mitihani kufanya mitihani tofauti na wanafunzi wengine.
Licha ya kubadilisha mtihani, alisema NECTA pia imekuwa ikiwakomoa wanaorudia kutokana na kuongeza alama ya ufaulu kutoka 41 hadi 51.
“NECTA iondoe kikwazo hiki kwani hii haina maslahi yoyote kwa maendeleo ya nchi hii. Kama haitaondoa tutegemee wanafunzi kufeli zaidi.
Mwisho       

Tuesday, November 23, 2010

BALOZI MAHIGA ALONGA KUHUSU SOMALIA

NA MAURA MWINGIRA, NEW YORK 
WATANZANIA wana mksemo mbalimbali ambayo hutumika kufikisha  ujumbe fulani. Moja ya misemo hiyo ni ‘mzigo mzito mpe Mnyamwezi’.
Msemo huo unasadifu na jukumu alilopewa aliyekuwa Balozi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Dk. Augustine Mahiga, la kuwa  mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa huko Somalia.
Ni heshima kubwa si kwa Balozi Mahiga kwa kuteuliwa kushika nafasi hiyo, lakini pia ni heshima kwa  Tanzania na Watanzania wote. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon katika angaza angaza yake,   hakumwona mtu mwingine wa kumkabidhi mzigo mzito, zaidi ya Balozi Mahiga.
Tayari Dk. Mahiga ameianza kazi hiyo ya kusimamia na kuhakikisha Somalia inakuwa na amani baada ya kuwa katika hali tete kwa takriban miaka 20 sasa.
 Baada ya kukabidhiwa jukumu lile, Balozi Mahiga alifungasha virago vyake na  kuhamia  Nairobi, Kenya ambako ndiko  ziliko ofisi zake.
Mwanzoni mwa Septemba, mwaka huu, Dk. Mahiga alifika mbele ya Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa, kutoa taarifa  yake ya kazi  ya kile ambacho amekiona, amekifanya na nini anashauri kifanyike. Katika taarifa yake, Balozi Mahiga  alianza kwa kutoa tahadhari kubwa kuhusu mwelekeo wa  nchi ya Somalia.
Alisema: “Kadri  Umoja wa Mataifa unavyoendelea kusuasua kuongeza kasi ya kuisaidia  serikali ya mpito ya Somalia, kuvisaidia vikosi ya kulinda amani vya Umoja wa Afrika  (AMISOM), kiintelejensia,  kijeshi kwa maana ya vifaa vya kisasa na askari wa kutosha wa kulinda amani, ndivyo Somalia inavyozidi kutumbukia katika kuwa kitovu cha ugaidi wa  kimataifa”,
Katika kauli yake hiyo, hakuzungusha  wala hakutaka kuremba maneno na kusema dalili za Somalia kuwa kitovu cha ugaidi zimekwishaanza kujitokeza na ziko wazi.
“Uzoefu unaonyesha  kwamba kadiri tunavyoendelea kuchelewa au kutoa ushirikiano mdogo kuhusu tatizo la Somalia, ndivyo hali inavyozindi kuwa ngumu na ya kutisha nchini humo. Lazima tuamue  sasa  kuzikabili  kwa dhati changamoto zinazoikabili Somalia,” alisema.
Alitahadharisha kuwa kuwepo kwa vitendo vya ugaidi wa kimataifa katika kanda ya Afrika ya Mashariki, kumejidhihirisha kwa matukio ya milipuko ya mabomu Kampala , Uganda Julai, mwaka huu  na shambulio la bomu liliofanyika  katika hoteli ya Muna , Somalia, wakati wa mwezi wa Ramadhani..
Kutokana na hali hiyo, alisema Umoja wa Mataifa kupitia Baraza lake la usalama,  hauna budi kuingilia kati kwa kukamata silaha na wapiganaji wanaoingia nchini Somalia kupitia bandari ya  Kismayu ambayo kwa sasa inashikiliwa na kundi la Al Shaabab
Somalia kwa miaka 20 sasa, imekuwa katika mapigano ya wenyewe kwa wenyewe na yake ya kikoo, yanayoendeshwa na wababe wa kivita, yakiwamo makundi ya kidini yenye misimamo mikali na ya kati.
Ndani ya muda huo, kumekuwa na serikali za mpito 19, ambazo zimekuwa zikianguka au kuangushwa moja baada ya nyingine. Ni Somalia hii ambayo dunia ilishuhudia matukio ya kutisha waliyofanywa na wanajeshi wa Marekani walioingia kujaribu kuweka sawa hali ya mambo.
Kwa sasa, Somalia si Somalia tena. Raia wake wametawanyika pembe zote za dunia, na huku mamia kwa maelefu wakiwa wakimbizi wa ndani ya nchi yao. Inajulikana katika jumuia ya kimataifa kama nchi iliyoshindikana. 
Lakini mbaya zaidi na ambalo  linaitisha  jumuia ya kimataifa, ni balaa la sasa ambalo nchi hiyo inaelekea kuwa kitovu  cha ugaidi. Hali hii  inaziweka mahali pagumu nchi za Afrika  Mashariki na za  Pembe ya Afrika.
Kupanuka kwa  ugaidi wa kimataifa, uharamia na  hali mbaya ya kibinadamu nchi Somalia, kunahitaji  nguvu  kubwa za ushirikiano kutoka jumuia  ya kimataifa. Pia inahitajika mkakati madhubuti wa kuzuia wimbi la uingizwaji wa silaha nchini humo.
Bandari ya Kismayu, kwa mujibu wa Dk. Mahiga, si tu inapitisha silaha haramu, bali pia inatumika kuingiza dawa za kulevya na wapiganaji wa kujitoa mhanga wanaotoka  mataifa mengine.
Kwa sasa, Somalia  iko chini ya utawala wa serikali ya mpito inayoongozwa na  Sheikh Sharif Sheikh Ahmed lakini kumekuwapo na   taarifa mbalimbali zinazoonyesha kuwa serikali hiyo ya mpito si tu kwamba haina nguvu au ubavu wa kupambana na makundi  yanayopingana nayo likiwamo kundi la Al Shabaa, bali pia kumekuwapo na mvutano na sintofahamu miongoni wa viongozi ndani ya serikali.
Udhaifu huo umefanya serikali hiyo inayosaidiwa na uwepo wa majeshi ya kulinda amani ya Umoja wa Afrika kutawala sehemu ndogo tu ya nchi hiyo. Kama hiyo haitoshi, kundi la Al Shabaab ambalo inasadikiwa kuwa na uwezo mkubwa kijeshi, limeendelea kuchukua maeneo mengi .
Baada ya jumuia ya kimataifa kushindwa kupeleka  wanajeshi wa kulinda amani Somalia,  viongozi wa Umoja wa Afrika waliamua kwa kauli moja kulibeba jukumu hilo. Uganda na Burundi zilikuwa nchi za mwanzo kutoa vikosi vyake.
Pamoja na nia hiyo njema, na kufanya kazi katika mazingira magumu, vikosi hivyo vinakabiliwa na changamoto nyingi zikiwemo za ukosefu wa zana za kisasa na askari kutolipwa mishahara kwa  wakati na kwa kiwango cha kuridhisha.
Hali hiyo imewafanya viongozi wa Afrika kupitia umoja wao, kuiomba   jumuia ya kimataifa hususani Umoja wa Mataifa kuviongezea nguvu vikosi hiyo.
Msimamo mkubwa wa viongozi hao ni kwamba jukumu la kuilinda Somalia, ni la Umoja wa Mataifa na si Afrika pekee. Viongozi hao wanaweka bayana kwamba Afrika iko yatari kutoa askari wa kutosha kwenda kupelea lakini ni lazima Umoja wa Mataifa utimize wajibu wake wa kusaidia kwa hali na mali.
Kauli hiyo ya viongozi wa Afrika, imepewa nguvu au kuongezewa uzito na Balozi Mahiga hasa aliposema: “Uwezo wa kijeshi wa vikosi hivi unahitaji kuimarishwa kwa kusaidiwa na jumuia ya kimataifa. Malipo kwa askari  lazima yalingane na ya wenzao walio katika operesheni zingine. Vikosi hivi vinahitaji vifaa vya kisasa vitakavyowawezesha kutekeleza majukumu yao hasa maeneo ya vijijini ambako mazingira yake ni magumu.”
Suala la kuitaka jumuia ya kimataifa kuongeza kasi ya kuvisaidia kwa hali na mali vikosi vya  Umoja wa Afrika  linapigiwa chapuo sana na viongozi wa ngazi zote  na hususan wale wanaotoka Afrika.
 Mawaziri wa Mambo ya Nje  wa Tanzania na Kenya kwa nyakati tofauti wamekuwa wakilipigia debe kwa nguvu zote umuhimu wa vikosi vya Umoja wa Afrika nchini Somalia kusaidiwa.
Kwa  mfano,  aliyekuwa Waziri wa mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania, Bernard Membe, amekuwa akisema Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa halina budi kusaidia jukumu hilo huku akisisitiza kuwa  mazingira magumu na ya hatari yanayowakabili wanajeshi wa  Burundi na  Uganda walioko Somalia, unaziogopesha nchi zingine kupeleka wanajeshi wake.
 “Kuna nchi sita zimejitolea kutoa wanajeshi ili kuongeza nguvu. Lakini  wanaona Waganda na Warundi wanavyoteseka, na hali hii inawatisha. Ni vyema basi jumuia ya kimataifa ikatekeleza mapema ahadi yake ya kutoka vifaa na fedha ili nchi nyingi zaidi zijitolee kupeleka watu wake,” alisisitiza Membe.
Alifafanua kuwa ingawa Afrika kupitia AMISOM imekwenda Somalia  kwa ajili ya kulinda amani, jukumu hilo si la Afrika peke yake bali ni la   jumuia ya kimataifa, kwa maana ya Umoja wa Mataifa.
Naye aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Moses Wentangula,  hakuwa nyuma katika kutilia mkazo  jambo   hilo pale aliposema: “Kama si majeshi ya Umoja wa Afrika  kutoa ulinzi kwa serikali ya mpito ya Somalia, hapana  shaka kwamba Al  Shaaba wangekuwa wameshaishika Somalia yote.”
Hata hivyo, alisema tatizo la Somalia si uwepo au wingi wa wanajeshi wa kulinda amani bali ni kukosekana kwa utashi kutoka jumuia ya kimataifa,  huku akionya kwamba ikitokea serikali ya mpito ya Somalia ikaangushwa na Al Shabaab kushika nchi, basi sehemu kubwa ya  eneo la Afrika Mashariki  na pembe ya Afrika itakuwa katika hatari.
Wetangula alisema ni matumaini yake kwamba kutokana na hali tete ilivyo ndani ya Somalia na tishio la ugadi wa kimataifa unaoibukia, hapana shaka jumuia ya kimataifa sasa itaamka na kuwajibika ipasavyo.
Hali tete na tishio la ugaidi wa kimataifa unaoibukia Somalia, si tu kwamba unawatia hofu viongozi wa Afrika hasa wale wa Afrika Mashariki na pembe ya Afrika, lakini kwa kuwa ugaidi huo umevaa sura ya kimataifa, unawatia hofu hata wakubwa wengine duniani.
Wakichangia taarifa ya Dk. Mahiga, wajumbe wa Baraza la Usalama si tu waliunga mkono hoja ya kutaka vikosi vya Afrika na serikali ya mpito  wasaidiwe, bali walionyesha  wasiwasi juu ya kuibuka wa ugaidi wa kimataifa ndani ya Somalia.
Kutokana na hali hiyo, walitaka na kutoa wito kwamba wakati umefika wa Umoja wa Mataifa  kutoa ushirikiano wa dhati kabla hali ya mambo haijafikia hali  ya kushindikana kabisa.
Hapana shaka kuwa Umoja wa Afrika umetimiza wajibu wake, na umekuwa tayari kuongeza vigosi ya kulinda amani hadi kufikia 2,000.  Lakini kama anavyosema Membe, moyo huo wa kujitolea wa Umoja wa Afrika utakwama kama jumuia ya kimataifa haitawajibika.

JIHADHARI UNAPOTUMIA LAPTOP


SAYANSI na teknolojia vimechochea kasi ya maendeleo ya sekta mbalimbali hivyo kuiwezesha jamii kupiga hatua katika nyanja anuai.

Maendeleo hayo kwa kiasi kikubwa yamechangiwa na uvumbuzi wa kila aina duniani.

Kompyuta ni moja ya nyenzo ambazo zimekuwa zikitumika katika sekta mbalimbali kwa lengo la kurahisisha ufanisi katika utendaji kazi.

Zana hiyo hutumika kwa ajili ya kuandika taarifa mbalimbali pamoja na kupata mawasiliano ya intaneti, ambayo huunganishwa na kompyuta.

Kuwepo kwa zana hiyo, kumeleta mageuzi makubwa duniani, ndiyo maana kuna msemo kwamba maendeleo katika sekta ya mawasiliano yameifanya dunia kuwa kijiji.

Katika eneo hilo, uvumbuzi ulianza kwa kutengeneza kompyuta kubwa za mezani lakini kazi hiyo iliboreshwa na kuanza kutengenezwa kompyuta za mkononi maarufu kama ‘laptop’.

Kompyuta hizo ndogo za mkononi, zimewezesha kurahisishwa kwa kazi na hata mawasiliano kwani mtu anaweza kutumia popote alipo na hata kutuma ujumbe au waraka duniani kote.

Aina hiyo ya kompyuta zinaweza kutumika mtu akiwa ofisini, baa, mgahawani, kwenye basi au kwenye meli. Mtu anayetumia anaweza kuweka mezani au popote anapoona panafaa na kumwezesha kufanya kazi yake bila matatizo.

Kwa watu wengi ambao huwa safarini au sehemu yoyote ambayo haina meza, huweka kifaa hicho kwenye mapaja na kuendelea na kazi zao. Kwa kufanya hivyo, hujisikia raha mustarehe na kazi hufanyika bila wasiwasi.

Pamoja na kompyuta hizo kurahisisha kazi, imeelezwa kuwa kuitumia huku ikiwa kwenye mapaja ni hatari kwa afya.

Awali, ilikuwa ikifahamika kuwa matumizi ya kompyuta kwa muda mrefu yanaweza kumfanya mtumiaji kupata matatizo ya macho na mishipa ya fahamu.

Lakini utafiti uliofanyika hivi karibuni, umebaini kuwa matumizi ya kompyuta ndogo kwa kuiweka kwenye mapaja husababisha ugonjwa wa ngozi na wakati mwingine saratani ya ngozi.

Madaktari waliofanya utafiti huo ambao matokeo yake yalitangazwa Oktoba, mwaka huu, hali hiyo husababishwa na joto la kompyuta hiyo. Joto la kompyuta hiyo hufikia hadi nyuzi joto  52.

Joto linalotokana na kompyuta hiyo, kwa mujibu wa watafiti hao na madaktari bingwa wa tiba ya binadamu, linaweza kusababisha mtumiaji kupata ugonjwa wa ngozi.

Wanasema ngozi ya mtumiaji huwa na vipele vidogo ambavyo baadaye husababisha mapaja kubadilika rangi au kuwa na vidonda.

Katika tukio la hivi karibuni, mtoto mwenye umri wa miaka 12 alikumbwa na madhara hayo katika paja lake la kushoto baada ya kutumia kompyuta ndogo kwa kucheza mchezo kwa saa kadhaa kila siku kwa zaidi ya miezi sita.
Matumizi kama haya ni hatari kwa afya yako. Chukua tahadhari ili usiungue mapajani.


“Kijana huyo alithibitisha kuwa kompyuta aliyekuwa akiitumia ilikuwa ya moto upande wa kushoto, lakini hata baada ya kugundua hakubadilisha namna ya kuiweka wakati wa kuitumia,” wanabainisha watafiti hao kutoka Uswisi katika jarida linalohusu tiba ya watoto.

Wanasema mwingine aliyekumbwa na madhara hayo ya kubabuka ngozi kwenye mapaja na rangi yake kubadilika ni mwanafunzi wa sheria nchini Marekani.

Mwanafunzi huyo ambaye ni msichana, alipopata tatizo hilo, kwa mujibu wa ripoti hiyo ya utafiti, alikwenda kuwaona madaktari wake wa ngozi.

Baada ya kwenda kwa ajili ya kumfanyia uchunguzi, madaktari wake walishangazwa na hali hiyo na walishindwa kubaini nini kilichomsibu. Lakini baadaye waligundua kuwa alipatwa na mkasa huo kwa sababu ya kutumia kompyuta ikiwa kwenye mapaja kwa muda wa saa sita kila siku.

Madaktari hao bingwa walifanya utafiti huo kuanzia mwaka 2007 na wamebaini kwamba watu wengi wameathirika na tatizo hilo.

Hata hivyo, wataalamu hao wakiongozwa na maprofesa Andreas Arnold na Peter Itin wa Chuo Kikuu cha Tiba cha Basel, Uswisi, wanasema tatizo hilo linaweza kuwa kubwa lakini ni vigumu kuelezea ni kwa kiasi gani kwa kuwa wengi hawajaripoti na kufanyiwa tiba.

Taarifa hiyo ya utafiti umewafikia watengenezaji wa kompyuta kama vile Apple, Hewlett Packard na Dell na wameonya kuwa ni hatari kutumia zana hizo zikiwa zimewekwa kwenye mapaja au katika ngozi ambayo haijafunikwa na kitu chochote.


KWA HILI CCM IJISAHIHISHA

OKTOBA 31, mwaka huu, ulifanyika uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, ambapo Rais Jakaya Kikwete, alichaguliwa tena kuongoza nchi.

Kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Rais Kikwete alipata kura 5,276,827 sawa na aslimia 61.17 ya kura zote halali zilizopigwa katika mikoa yote 26 ya Tanzania.

Wagombea wengine waliojitokeza kugombea nafasi hiyo ni Dk. Willibrod Slaa (CHADEMA), Profesa Ibrahim Lipumba (CUF), Hashim Rungwe (NCCR Mageuzi), Peter Mziray (APPT Maendeleo), Fahmi Nassor Dovutwa (UPDP) na Mugahywa Muttamwega wa TLP).

Katika kinyang’anyiro hicho, Dk. Slaa alipata kura 2,271,941 (asilimia 26.34), Profesa Lipumba kura 695 (asilimia 8.06), Fahmi Nassoro Dovutwa kura 13,176 (asilimia 0.15), Peter Mziray kura 96,933 (asilimia 1.12), Hashim Rungwe kura 26,388 (asilimia 0.31) na Mugahywa Muttamwega kura 17,482 sawa na asilimia 0.20.   

vile vile, katika uchaguzi wa Wabunge na Madiwani, CCM ilizoa viti vingi hivyo kupata nafasi ya kuunda serikali kwa maana ya serikali kuu na halmashauri za majiji, manispaa, miji na wilaya. Hata hivyo, ziko sehemu chache ambazo vyama vya upinzani vilifurukuta hivyo kupata fursa ya kuunda halmashauri.

Pamoja na kupata ushindi huo wa kishindo, matokeo ya mwaka huu yameleta hisia tiofauti kwani CCM imepoteza viti vya ubunge na udiwani katika maeneo ambayo ilikuwa ikiyashikilia.

Hata katika kura za urais, Rais Kikwete alipata kura chache kulinganisha na alizopata mwaka 2005. katika uchaguzi wa mwaka 2005, Rais Kikwete alipata kura 9,123,952 sawa na asilimia 80.2 ya kura halali zilizopigwa, akifuatiwa kwa mbali na Profesa Ibrahim Lipumba wa CUF ambaye alipata kura 1,327,125 (asilimia 11.7).

Kitarakimu, kura alizopata Rais Kikwete, zimepungua kwa kiasi cha kura 3,846,125 kulinganisha na zile za mwaka 2005, licha ya kwamba waliojitokeza mwaka huu walikuwa wachache tofauti na uchaguzi uliopita.

Kwa upande wa ubunge, baadhi ya maeneo ambayo imepoteza ni (Ilemela, Nyamagana na Ukerewe (Mwanza), Mbeya Mjini na Mbozi Magharibi (Mbeya) na Karatu na Arusha Mjini (Arusha).

Mengine ni Vunjo, Rombo na Hai (Kilimanjaro), Kilwa Kusini na Lindi Mjini (Lindi), Iringa Mjini (Iringa), Kigoma Kusini, Muhambwe, Kasulu Mjini na Kasulu Vijijini (Kigoma), Biharamulo (Kagera), Maswa Magharibi, Maswa Mashariki, Bukombe na Meatu (Shinyanga).

Pia CCM imepoteza Mbulu (Manyara), Biharamulo (Kagera), Singida Mashariki (Singida), Kawe na Ubungo (Dar es Salaam) na Musoma Mjini (Mara).

Vile vile kwa visiwani, imepoteza majimbo matatu ya Magogoni, Mwanakerekwe na Mtoni nap ia kushindwa kukomboa jimbo la Mji Mkongwe lililo katika himaya ya CUF.

 Pamoja na kupoteza majimbo hayo, CCM imefanikiwa kukomboa jimbo la Tarime lililokuwa chini ya CHADEMA miaka mitano iliyopita.

Hata hivyo, CCM imeshindwa kuyakomboa majimbo ya Mpanda Mjini, Moshi Mjini ambayo yamekuwa yakishikiliwa na CHADEMA, Mji Mkongwe (CUF), Bariadi Mashariki (UDP) na mengine 18 ya Pemba.

CHANZO NINI?
Kupoteza majimbo mengi kwa kiasi hicho, kumesababisha mjadala miongoni mwa wachambuzi na hata baadhi ya watu kuanza kudhani kuwa mustakabali wa uhai wa CCM sasa uko shakani.

Zipo sababu nyingi zilizofanya kuwepo kwa hali hiyo ambazo CCM inapaswa kuzifanyia kazi ili kuhakikisha yaliyotokea hayajirudii katika uchaguzi ujao.

Sababu kubwa iliyofanya majimbo mengi kwenda upinzani, na pengine kubwa kuliko zote, ni ubinafsi miongoni mwa viongozi hasa watendaji katika ngazi za wilaya na mikoa.

Watendaji hao, yaani makatibu wa mikoa, wilaya pamoja na wale wa jumuia za Chama, walishiriki kukihujumu chama hasa kwa kupendelea baadhi ya wagombea. Mfano katika hilo ni Dar es Salaam na Iringa.

Mkoani Dar es Salaam wana CCM katika majimbo ya Kawe na Ubungo waliamua kuwapigia kura wagombea wa CHADEMA na kuwatosa wale wa CCM.

Sababu kubwa iliyotolewa na wanachama hao ni kwamba wagombea wa CCM, Hawa Ng’humbi (Ubungo) na Angela Kizigha (Kawe) hawakuwa chaguo bali la viongozi wa Chama. Chaguo lao, kwa mujibu wa wanachama hao, walikuwa Nape Nnauye na Kippi Warioba.

Licha ya ubunge, suala la viongozi kuchakachua matokeo lilijitokeza katika kura za maoni za udiwani ambapo katika baadhi ya kata jijini Dar es Salaam waliopendekezwa si wale walioshinda katika kinyang’anyiro hicho.

Hiyo ilijidhihirisha katika kata za Miburani, Chang’ombe na Wailesi (Temeke) na Msewe (Ubungo) ambapo wanachama waliandamana hadi ofisi za CCM Mkoa kulalamikia uchakachuaji wa matokeo.

Katika kata ya Miburani, kwa mfano, wanachama waliandamana kumkataa Fortunatus Mang’wela (aliyekuwa diwani kabla ya kura za maoni) kwa madai kuwa hakuwa chaguo lao bali waliyemchagua alikuwa Juma Mkenga.

Mkoani Iringa nako, kulikuwa na kizaazaa katika majimbo ya Iringa Mjini na Kalenga. Kalenga, kwa mfano, aliyekuwa Katibu wa CCM wa Wilaya ya Iringa Vijijini, Luciano Mbossa alidaiwa kumpendelea wazi wazi Abbas Kandoro  wakati wa kura za maoni.

Ilidaiwa kuwa katibu huyo kwa kushirikiana na baadhi ya watendaji katika wilaya kwa maana ya viongozi wa Chama na jumuia, na wajumbe wa kamati ya Siasa ya Wilaya, walifanya kila njia kuhakikisha Kandoro anashinda.

Hata matokeo yalipotoka na kuonyesha kuwa mgombea waliyembeba ameshindwa dhidi ya Dk. William Mgimwa, bila aibu, walianza kupita usiku kwenye baadhi ya kata na kubadilisha matokeo ili mtu wao aonekane ameshinda.

Azma yao hiyo ilifanikiwa na kumtangaza Kandoro kuwa mshindi. Lakini kutokana na Dk. Mgimwa kujua ndiye aliyeshinda, alisimama kidete na kuhakikisha haki inatendeka na hatimaye kutangazwa mshindi.

Jambo kama hilo pia lilijitokeza katika jimbo la Iiringa Mjini ambapo viongozi wa CCM wilaya kwa kushirikiana na baadhi ya watendaji wa mkoa chini ya Katibu wa Mkoa, Mary Tesha,  walimwengua Frederick Mwakalebela aliyekuwa ameshinda na kumpendekeza Monica Mbega.                    
       
Viongozi hao walifanikiwa kuishawishi Kamati ya Siasa ya Mkoa na vikao vya Chama ngazi ya taifa kumwengua mshindi huyo wa kura za maoni. Madai waliyoyatoa ni kujihusisha na vitendo vya rushwa.

Hali hiyo iliwashangaza wananchi wengi wa jimbo la Iringa na kuapa kuwa uonevu huo dhidi ya mgombea wao wataulipizia kwa njia ya kura. Ndivyo walivyofanya katika kura kama waklivyoahidi kwa  kumchagua Mchungaji Peter Msigwa wa CHADEMA. Kwa kufanya hivyo, CCM ikakosa mwana na maji ya moto.

UAMUZI WA WANANCHI
Kwa kawaida viongozi wanachaguliwa na wananchi, kama misingi ya demokrasia inavyobainisha. Kwa mantiki hiyo, uamuzi wa wananchi unapaswa kuheshimiwa na ndivyo CCM ilivyopaswa kufanya hivyo.

Hiyo pia ilielezwa bayana na viongozi wa ngazi za juu wa CCM wakiwemo Mwenyekiti Rais Kikwete na makamu wake, Pius Msekwa. Viongozi hao walisema Chama kitaheshimu uamuzi wa wananchi na kwamba watakaoshinda kwenye kura za maoni, ndio watakaopitishwa kugombea.  

Ni kweli katika maeneo mengi, CCM ilifanya hivyo. Lakini katika baadhi ya maeneo watu waliolalamikiwa kuwa ama walishinda kwa mizengwe au kubebwa na viongozi wa mikoa na wilaya, walipitishwa.

Hatua hiyo iliwafanya wanachama kuwapigia kura wagombea wa upinzani, ikiwa ni majibu kwa Chama kutokuheshimu matakwa yao.         

Mfano dhahiri ulioonyesha kuwa wananchi waliamua kuihukumu CCM ni katika jimbo la Bukombe, Shinyanga, ambapo Profesa Kulikoyela Kahigi, aliyejiengua CCM na kuhamia CHADEMA baada ya kura za maoni, aliibuka kidedea dhidi ya Emmanuel Luhahula ambaye alilalamikiwa kuwa hachaguliki lakini Chama kilimpitisha.

Hali hiyo pia ilitokea katika Maswa Magharibi ambapo baadhi ya viongozi wa mkoa na wilaya walimfanyia mizengwe John Shibuda, aliyekuwa mbunge. Shubuda alijiunga na CHADEMA na hatimaye wananchi kumpa ridhaa ya kurejea bungeni.

KUZINGATIA UTAFITI
Jambo lingine ambalo limesababisha CCM kupoteza majimbo mengi, ni kutokufanyia kazi taarifa mbalimbali zikiwemo za utafiti kama ile ya Mpango wa Utafiti wa Elimu na Demokrasia (REDET) wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

REDET, katika utafiti wake, ilieleza kuwa wabunge 143 kati ya 232 waliokuwemo katika bunge lililopita kutoka majimbo ya uchaguzi hawachaguliki, hivyo kuwa vigumu kurejea bungeni baada ya uchaguzi mkuu.

Utafiti wa taasisi hiyo, iliyo chini ya Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala ya Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, ulionyesha kuwa  asilimia 61.7 ya wabunge wasingechaguliwa tena. Kwa upande wa Rais pia, ilielezwa kuwa Rais Kikwete angeweza kupata asilimia 66.9.

Sababu kubwa iliyotolewa na wananchi waliohojiwa ni utendaji wa wabunge hao majimboni Kwa maana hiyo, wananchi walionyesha kuchoshwa na utendaji wao na kwamba wanaridhika nao kwa asilimia 38.

Matokeo ya uchaguzi wa Oktoba 31, mwaka huu kwa kiasi fulani, yamelingana na utafiti wa REDET kwani Rais amepata asilimia 61.17 ambayo ni tofauti ya asilimia 5.73. Wabunge wa zamani ambao hawakurudi majimboni ni asilimia  57.7, ambayo ni tofauti ya asilimia nne kulinganisha na ile ya REDET.

Kutokana na taarifa za utafiti kama ile ya REDET, CCM ilipaswa kuifanyia kazi na kuhoji ni kwa nini inatokea hivyo, badala ya kuamini tu kuwa itaibuka na ushindi wa kishindo kama si wa mafuriko.  

MAKUNDI HATARI
Ndani ya CCM, kuna makundi ya wanachama na viongozi, jambo ambalo ni sababu ya kushindwa kwa Chama katika baadhi ya nafasi kwenye uchaguzi.

Mkoani Iringa, kwa mfano, kuna kundi linaloundwa na wanasiasa na wafanyabiashara walioko ndani na nje ya mkoa huo, maarufu kama ‘Iringa Network’. Kundi hilo, kwa mtazamo wake, linadhani bila wao hakuna kinachoweza kufanyika na kwamba wao ndio Iringa na Iringa ni wao.

Mtu anapotaka kugombea ubunge, mathalan, anatakiwa awaone ndipo apate baraka zao. Vile vile, kundi hilo huhakikisha kila mtendaji (makatibu wa mkoa na wilaya) anayepelekwa huko, anawekwa mikononi mwao na kutekeleza matakwa yao.   

Watu hao ndio waliochangia kwa kiasi kikubwa CCM kupoteza jimbo la Iringa Mjini. Ndio waliohakikisha kwa gharama zozote Mwakalebela anaenguliwa. Walifanikiwa lakini nguvu ya wananchi iliwapa fundisho kwa mgombea wao kupigwa chini.

Makundi kama ‘Iringa Network’ yapo kila sehemu na hayo ni sumu kubwa kwa ustawi na maendeleo ya Chama katika ngazi zote. Kuendelea kwa makundi kama hayo kunaweza kukimaliza Chama.   

Licha ya makundi, ili kubadilika, CCM haina budi kwenda hali halisi ya sasa. Ni lazima itambue kuwa kizazi cha sasa ni tofauti na cha miaka 10 au 15 iliyopita, na hiyo ni changamoto kubwa.

Uelewa katika kizazi cha sasa uko juu kulinganisha na miaka 10 hadi 15. Kuna ongezeko kubwa na wasomi kutokana na kuibuka kwa vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu, hivyo uwezo wa kupembua na kuchanganua mambo umeongezeka. Kwa mantiki hiyo, CCM lazima ihame kutoka mtandao wa ‘analogue’ na kwenda kwenye ‘digital’.

Ni dhahiri kwamba kama CCM itatekeleza na kujisahihisha katika mambo haya na mengine, Watanzania watajenga imani zaidi na kuendelea kuichagua. Kinyume cha hapo mambo yatakuwa tofauti.